Image

Upasuaji wa moyo duniani

Historia ya upasuaji wa moyo

Mapinduzi na maendeleo makubwa katika tiba ya upasuaji wa moyo duniani yanaanzia mwaka 1944 wakati kwa mara ya kwanza duniani katika Hospitali ya John Hopkins nchini Marekani ilifanyika operesheni ya kwanza ya upasuaji wa moyo na kufanikiwa kwa mtoto aliyekuwa na tatizo la moyo la kuzaliwa nalo lililokuwa linasababisha watoto watoto kufa kwa kukosa hewa safi ya oksijeni katika mzunguko wa damu mwilini.

Operesheni hii ilifanywa na Dkt. Alfred Blalock na wanafunzi wake wa upasuaji akiwemo Dkt. Denton A. Cooley (Mwalimu wangu na mwanzilishi wa Texas Heart Institute ya Marekani) baada ya kuombwa na daktari wa watoto, Dkt. Hellen Taussing kujaribu kuokoa maisha ya watoto hao waliokuwa wanakufa bila ya kujua jinsi ya kuwasaidia.

Lakini la muhimu kutambua ni kuwa, operesheni hii ya kwanza duniani ilifanikishwa na kijana Mmarekani mweusi (African-American), Vivien Thomas aliyekuwa msaidizi wa Dkt. Alfred Blalock kwa majaribio ya kisayansi aliyewezesha kufanyika kwa operesheni hii na akafikia kupewa Udaktari wa Heshima (Honorary Doctor of Medicine) na kufundisha madaktari wengi wa upasuaji wa moyo waliopitia katika Hospitali ya John Hopkins. Hivyo operesheni hii huitwa ‘Blalock-Taussing Shunt’. Lakini historia itamkumbuka Dkt. Vivien Thomas kwa mchango wake.

Operesheni hii ilikuwa ni ya kuunganisha baadhi ya mishipa ya damu ili kuwezesha mwili wa mtoto kupata hewa safi. Ingawa operesheni hii ilikuwa si ya kufungua moyo moja kwa moja lakini ilisaidia kutoa mwanga kuwa inawezekana kuufanyia moyo upasuaji na kurekebisha kasoro zilizo ndani ya moyo.

Hivyo madaktari na wanasayansi waliendelea na majaribio mbalimbali kwa kutumia wanyama na hadi baada ya vita ya Pili ya Dunia ambapo baadaye Dkt. John Gibbon na mkewe Mary Gibbon katika chuo kikuu cha Minnesota mjini Minneapolis nchini Marekani walipofanikiwa kugundua mashine ya

kupitisha damu nje ya moyo (Heart-Lung machine/ Extracorporal Circulation machine au Cardiopulmonary Bypass machine) na kuweza kufanya operesheni kwa kuupasua moyo na kurekebisha kasoro zilizo ndani yake. Hapa ndipo mapinduzi makubwa na maendeleo makubwa katika tiba yalianza kutokea. Hii ilikuwa ni mwaka 1953.

Upasuaji wa moyo wa kisasa ulianza na mabingwa wengi zaidi kujitokeza kama kina Dkt. Lillehei, Denton A. Cooley, Michael De Bakey, John Kirkin, Crafoord, Francis Fontan na wengineo wengi.

Mwaka 1967 operesheni ya kwanza ya ya upasuaji wa moyo duniani kwa kupandikiza/ kuweka moyo wa mtu mwingine (Heart Transplant) ulifanyika huko nchini Afrika Kusini na Dkt. Christian Barnard. Mwaka mmoja baadaye, yaani mwaka 1968, operesheni ya kwanza duniani ya upasuaji wa moyo kwa kumuwekea mgonjwa moyo wa bandia (Artificial Heart Transplant) ilifanywa na Dkt. Denton Cooley (mwalimu wangu na mwanzilishi wa Texas Heart Institute) mjini Houston, Texas, Marekani.

Kufanyika na kufanikiwa kwa upasuaji huu kulileta changamoto na maendeleo makubwa katika tiba kwa ujumla na hasa katika tiba ya moyo na upasuaji wa moyo. Kwa hivi sasa, sayansi ya tiba ya moyo imekua kiasi kwamba leo hii tupo kwenye upasuaji wa kutumia mirija (catheterization/ Angioplasty), kwa kukata kidogo bila kuharibu mwili au moyo (minimally Invasive Surgery) na kwa kutumia vifaa bandia (Robbotic Surgery).

Lakini pamoja na maendeleo haya duniani, Bara letu la Afrika ikiwemo nchi yetu Tanzania sayansi hii inaonekana ni kama ndoto. Kuna kila haja ya kufanya juhudi za ziada ili bara letu na hasa nchi yetu ya Tanzania iweze kufikia hapo wenzetu walipofikia. Tazama takwimu za upasuaji wa moyo zilizivyo duniani katika karne hii ya 21.

Takwimu za upasuaji moyo duniani

Kama zilivyotolewa na Shirika na Moyo Duniani  (World Heart Foundation) mwaka 2002

  • Operesheni za moyo 860 kwa kila idadi ya watu milioni moja hufanyika Marekani ya Kaskazini, Australia na Ulaya
  • Operesheni zamoyo 60 kwa kila watu milioni moja hufanyika Amerika ya Kusini, Urusi, Asia na Afrika
  • Hii inamaanisha kuwa takribani 93% ya watu wanaohitaji huduma ya upasuaji wanaoishi nje ya Amerika, Australia na Ulaya hawapati huduma hii
  • Kwa takwimu halisi ni kwamba, watu karibu bilioni 4.5 duniani hawafikiwi na huduma ya upasuaji wa moyo duniani.

Changamoto ya Uwezo wa Upasuaji wa Moyo

Teknolojia hii ina changamoto zake kadhaa zikiwemo

  • Ni sayansi ya kisasa zaidi, hivyo
  • Ina gharama – vifaa ni aghali sana, na
  • Kuna upungufu wa wataalamu, ambao kwa upande fulani husababishwa na
  • Kutokana na kukosa mtazamo
  • Kuanisha mradi mpya hakuwavutii wafadhili/ wakopeshaji kwa vile faida huchukua muda mrefu zaidi kupatikana kama miaka zaidi ya mitano, na
  • Mgongano wa maslahi kama vile kitendo cha kupeleka wagonjwa nje ya nchi huwanufaisha sana baadhi ya watu, lakini pia
  • Ni ngumu kwa watu wa kawaida kumudu gharama za tiba ya upasuaji wa magonjwa haya

Dkt. Ferdinand B. Masau ni Daktari Bingwa wa Tiba na Upasuaji wa Moyo katika Taasisi ya Moyo Tanzania (THI). Makala hii inapatikana pia katika kitabu chake cha “Magonjwa ya Moyo, Yajue, Yazuie na Yatibu”.

Imesomwa mara 5952 Imehaririwa Jumatatu, 15 Mai 2017 15:11
Dr Fabian P. Mghanga

Daktari bingwa na Mhadhiri katika kitivo cha Afya Chuo Kikuu Kishiriki cha Askofu Jacob, Songea

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.

Makala shabihana