Image

Wanasayansi China Wagundua Bakteria aina ya E.coli Wanaosababisha Vifo Barani Ulaya

Kwa wiki tatu mfululizo bara la ulaya limekumbwa na janga la bakteria aina ya E.coli ambao wako tofauti na E.coli wale wanafahamika duniani kote na hivyo kusababisha vifo vingi sana barani ulaya.

Wanasayansi nchini China kutoka katika kitengo cha utafiti cha Beijing Genomics Institute (BGI), ambacho ndicho kituo kikubwa zaidi cha kufanya utafiti wa mambo ya vina saba (DNA) duniani kote, alhamisi ya tarehe 2 /6/ 2011 walitangaza kugundua aina hii mpya ya E.coli.

Watafiti hao ambao walipata chembechembe za vina saba kutoka kwa wanasayansi wa Ujerumani ambao wana ushirikiano nao wa karibu, waliweza kutambua bakteria hawa kwa muda wa siku tatu tu na hivyo kuwafanya kuwa wa kwanza kabisa duniani kugundua aina hii mpya ya E.coli na pia wakaweka muundo mzima wa vina saba (full sequence) wa bakteria hawa kwenye mtandao.

Pia waliweza kugundua viashiria vya asili (genes) ambavyo vinawasaidia bakteria hawa kuwa vigumu kuwaua kwa kutumia aina kuu tatu za dawa za antibiotics zinazojulikana kuua bakteria aina ya E.coli na hivyo kuweza kutoa jibu la kwa nini madaktari katika bara la ulaya wana wakati mgumu kukabiliana na janga hili la E.coli ambalo limeshaua watu 17 na wengine 1500 wakiugua kutokana na janga hili.

“Tumefanya uchunguzi zaidi na kugundua viashiria vya asili (genes) zaidi ambavyo si rahisi kuangamizwa kwa antibiotics na vyenye sumu kali, kazi yetu bado inaendelea” alisema Qi Junjie, mmoja wa wanasayansi hao wanaohusika na utafiti huo. Dawa ambazo wanasayansi kutoka China wamegundua hazina uwezo wa kuua bakteria hawa, ni zile ambazo hutumiwa mara kwa mara kutibu magonjwa yanayoathiri tumbo na wanazopewa wagonjwa baada ya kufanyiwa upasuaji kama kinga dhidhi ya bakteria hawa aina ya E.coli hatari sana.

“Hii inamaanisha madaktari wana zana chache sana kukabiliana na janga hili jipya la bakteria hawa wa E.coli” alisema William Chui, makamu wa rais wa kikundi cha wafamasia wa hospitali cha nchini Hong Kong, ambaye yeye hakuhusika katika utafiti huu. Barani ulaya, mamkala bado zinajitahidi kutafuta chanzo cha mlipuko/janga hili ambapo wanaamini kusambazwa kupitia mboga za majani pamoja na matango mabichi.

E.coli ni nini?

Escherichia coli au E.coli kwa kifupi ni bakteria ambao hupatikana kwenye utumbo mdogo wa binadamu, kuna aina nyingi za E.coli ambazo baadhi yake hazina madhara yoyote kwa binadamu isipokuwa baadhi ambazo huweza kusababisha magonjwa hatari kama food poisoning, ugonjwa wa maambukizi katika njia ya mkojo (UTI), ugonjwa wa uti wa mgongo kwa watoto wachanga (neonatal meningitis), hemolytic uremic syndrome, peritonitis, mastitis, septicaemia na Gram - negative pneumonia (homa ya mapafu).

Zile aina ambazo hazina madhara kwa binadamu, husaidia katika kutengeneza vitamin K2 kwenye utumbo wa binadamu na hivyo kumlinda mtu kupata maambukizi ya aina za E.coli zenye madhara mwilini. E.coli huwa wanapatikana zaidi kwenye kinyesi na huenezwa kwa kula chakula ambacho kimechanganyikana na kinyesi. E.coli ni kati ya bakteria wanawaofanyiwa utafiti zaidi kwenye maabara kwa muda wa miaka 60 hadi sasa kwani utafiti wake hauna gharama sana. Bakteria hawa waligundulika na mwanasayansi wa ujerumani ambaye pia alikuwa dakatri wa watoto anayeitwa Theodor Escherich mwaka 1885 na kupewa jina la E.coli kama heshima na kumbukumbu ya kumuenzi mwanasayansi huyu.

Kituo Kikubwa Kabisa Duniani cha Utafiti wa Vinasaba (DNA)

Aina hii mpya ya E.coli iliyogundulika inafanana na zile aina nyengine zinazosababisha ugonjwa wa kuhara damu, hemolytic uremic syndrome ambao huathiri figo. “Aina hii mpya ni ya ajabu sana, viashiria vyake vya asili vimekopwa kutoka katika aina zile nyengine na hivyo kuvipa uwezo wa kusababisha ugonjwa wa kuhara damu na ugonjwa wa hemolytic uremic syndrome” alisema Qin, makamu rais wa kituo cha utafiti wa vina saba BGI Microbiology Trasnformic centre.

Kwa wengi kujihusisha kwa China kugundua aina hii mpya ya E.coli ni ajabu sana kwao, kwani bado wanakumbukumbu ya jinsi nchi hiyo ilivyojaribu kuficha janga la ugonjwa hatari wa mapafu SARS mwaka 2003. Lakini kwa watafiti wengi, nchi ya China imepitia mageuzi makubwa kutoka mwaka 2003 hadi sasa.Kitengo cha BGI cha utafiti kilichopo mjini Shenzhen, kilomita 7,000 kutoka barani ulaya, kinapata ufadhili mkubwa kutoka serikali ya China ambayo ni tajiri sana.

“Kitengo cha BGI kina mashine 180 na wafanyakazi 4,000 na hivyo kukifanya kuwa kitengo kikubwa kabisa na cha kwanza cha aina yake duniani” alisema Yang Bichen, mkurugenzi masoko wa kituo hicho. Kwa utambuzi wa viashiria vya asili (DNA sequencing alone) tuna watafiti 300” alisema Bi Yang Bichen wakati akiongea kwenye simu na shirika la habari la Reuters hapo ijumaa.

“Bado tunajaribu kuelewa viashiria vya asili venye sumu (toxic genes) vya bakteria hawa wapya (E.coli) pamoja na kufanya utafiti juu ya kazi ya viashiria hivyo (toxic genes)” alisema Bi Yang Bicheng, ambaye ni mwanasayansi kitaaluma.

“Tunafanya majaribio ya vifaa ambavyo vitaweza kugundua/kuchunguza bakteria hawa hospitalini na majumbani na tunataraji kupata kibali karibuni ili viweze kutumika kugundua E.coli kwenye chakula na kwa binadamu” aliendelea kusema Bi Yang. Kitengo cha BGI kilichopo shenzhen kinajihusisha na tafiti za vina saba (DNA sequencing) na pia hutoa huduma nyengine za utafiti kwa jumuiya ya wanasayansi na watu binafsi, faida inayopatikana kutokana na huduma hizo inatumiwa katika utafiti na maendeleo ya kituo hicho.

Mbali na kufanya tafiti za vina saba, kituo cha BGI, kinajihusisha na utafiti wa kuzalisha wanyama kwenye maabara (animal cloning) na kutengeneza mbegu bora za mchele na mbegu nyengine za kilimo ambapo China inatarajia kupata uwezo wa kuwalisha wananchi wake wanaongezeka idadi kila mwaka kutokana na utafiti huo.

Wanasayansi wa kituo hicho cha BGI, ambao wengi wao wamesomeshwa katika vyuo bora kabisa barani ulaya na Marekani, wameboresha na kugundua njia zao wenyewe za kuzalisha wanyama kwenye maabara na kuwajengea uwezo wanasayansi wake ambapo kila mmoja ana uwezo wa kupandikiza mayai 200 ya nguruwe kwa siku. Karibuni, BGI kimezindua kitengo cha kuhamasisha watu kuzalisha wanyama kwenye maabara pamoja na kutumia nyama zinazotokana na wanyama wanaozalishwa maabara, na kinatarajia nyama hiyo kuwepo kwenye soko nchini China miaka michache ijayo.

Changamoto kwa wanasayansi na serikali

Ni matarajio yetu ya kwamba utafiti huu utatoa changamoto kwa serikali kuona umuhimu wa kufanya utafiti katika nyanja mbalimbali pamoja na kuwajengea uwezo wanasayansi tulionao. Juhudi za makusudi ni lazima zichukuliwe kuboresha maslahi ya wanataaluma, ambayo ni pamoja na mishahara mizuri, mazingira mazuri ya kufanyia kazi, vifaa vizuri, kuwaendeleza kielemu pamoja na kuthamini tafiti wanazofanya kwa kuzifanyia kazi nchini na kuacha au kupunguza utegemezi wa teknolojia kutoka nje ya nchi. Pia wanasayansi hawana budi kuwa wabunifu zaidi katika kuboresha teknolojia pamoja na kubuni zile ambazo zitaweza kutumika katika mazingira ya nchi yetu.

"We wish to suggest a structure for the
salt of deoxyribose nucleic acid
(D.N.A.). This structure has novel features
which are of considerable biological interest." -
Watson and Crick, Nature, 25 April 1953

Maneno halisi waliyotamka wanasayansi Watson na Crick wakati wa utambulisho wa mchoro wao wa vina saba mwaka 1953.

Imesomwa mara 4828 Imehaririwa Alhamisi, 18 Mai 2017 13:17
Dr Khamis

Dr. Khamis H.Bakari (MD PhD) ni daktari bingwa,mhadhiri katika chuo cha afya cha Chuo  Kikuu cha Dodoma,mtaalamu wa Tiba na Uchunguzi kwa kutumia mionzi ya nyuklia (Nuclear medicine).

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.

Makala shabihana