Image

Unywaji Chai Kwa Wingi ni Hatari kwa Afya?

Mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 47 kutoka jimbo la Michigan nchini Marekani amepata ugonjwa adimu sana(rare disease) wa mifupa baada ya kunywa chai iliyotengenezwa kwa aina mia moja ya majani ya chai kwa wingi (lita 3 kwa siku) kwa miaka 17 mfululizo, watafiti kutoka Marekani wamesema.

Mwanamke huyo alikwenda hospitali kuonana na Daktari baada ya kuwa na maumivu makali kwenye kiuno,mikono,miguu na kiuno kwa miaka mitano.

Baada ya kufanyiwa kipimo cha X-ray iligundulika mama huyo ana ugonjwa huo adimu ambao huonyesha dalili za kuongezeka kwa uzito wa mifupa ya uti wa mgongo(dense spinal vertebrae) pamoja na kushikana(calcifications of ligaments) kwa viunganishi vya mifupa ya kwenye mikono’’ alisema mmoja wa watafiti Dr. Sudhaker D. Rao, Daktari bingwa wa magonjwa vichocheo vya mwili na virutubisho vya mifupa na vya mwili (Endocrinologist and bone and mineral metabolism physician) katika hospitali ya Henry Ford Hospital,Marekani.

Dr. Rao alihisi mama huyo ana ugonjwa wa mifupa unaojulikana kama skeletal fluorosis unaosababishwa kwa kutumia kwa wingi madini aina ya fluoride (Fluoride hupatikana kwenye maji au chai)

Kiwango cha madini ya fluoride katika damu ya mama huyo kilikuwa juu mara nne zaidi ya kiwango kinachohitajika kwenye mwili wa mwanadamu.

Ugonjwa wa skeletal fluorosis huonekana sana kwenye maeneo ambayo kiasili yana madini ya fluoride kwa wingi kama baadhi ya maeneo nchini India na China (katika nchi nyingi kiwango kidogo cha fluoride huweka kwenye maji, dawa za meno kama kinga dhidhi ya ugonjwa wa meno unaojulikana kama cavities)

‘’Mgonjwa alipewa rufaa ya kuja kuniona kwa sababu madaktari walie muona mwanzo walidhani ana saratani ya mifupa, lakini baada ya mimi kuona X-ray za mgonjwa,mara moja nilitambua kuwa ni ugonjwa wa skeletal fluorosis kutokana na kuwahi kuona wagonjwa wa aina hiyo nilipokuwa kwetu nchini India’’alisema Dr. Rao

‘’Kwa kawaida mwili huchukua kiwango cha madini ya fluoride kinachohitajika tu na kiwango chochote cha ziada hutolewa kupitia kwenye figo.Iwapo mtu atakunywa fluoride nyingi kama mgonjwa huyu alivofanya kutokana na tabia yake ya kunywa chai kwa wingi,basi baada ya muda mrefu madini haya ya fluoride hujikusanya kwa pamoja na kujipandikiza kwenye mifupa’’ aliendelea kusema Dr. Rao.

Dr. Rao alisema huko nyuma waliwahi kupata wagonjwa wengine wachache wa skeletal fluorosis ambao walikuwa wakinywa lita 3.7 za chai kwa siku na baada ya kuwaambia wagonjwa hao waache kunywa chai, dalili za ugonjwa huo zilianza kupungua na wagonjwa kupata nafuu kubwa.

Mkusanyiko wa madini ya fluoride kwenye mifupa hupotea baada ya muda mrefu ikiwa mgonjwa ataacha kunywa chai kwani mifupa ina kawaida ya kujirekebisha (bone repair) yenyewe baada ya muda.

Utafiti huu unapatikana katika jarida la New England Journal of Medicine liliochapwa tarehe 21 march 2013. Madini ya fluoride hupatikana kwa wingi katika maeneo ya kaskazini mwa Tanzania.

Kwa wale wanaopenda kunywa chai basi wajitahidi wasinywe zaidi ya vikombe tano kwa siku.

 

 

 

Imesomwa mara 5389 Imehaririwa Alhamisi, 08 Novemba 2018 16:56
Dr Khamis

Dr. Khamis H.Bakari (MD PhD) ni daktari bingwa,mhadhiri katika chuo cha afya cha Chuo  Kikuu cha Dodoma,mtaalamu wa Tiba na Uchunguzi kwa kutumia mionzi ya nyuklia (Nuclear medicine).

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.

Makala shabihana