Siku zote madaktari wanashauri kina mama wajawazito kulala ubavu mmoja hasa upande wa kushoto ili kuepuka kuzaa mtoto mfu au mtoto mwenye uzito mdogo kwa sababu mwanamke mjazito anapolalia ubavu wake wa kushoto huongeza mzunguko wa damu kwa kiumbe kilichomo ndani yake.
Utafiti huu uliofanyika nchini Ghana unaunga mkono utafiti uliofanyika hivi karibuni nchini Australia unaojulikana kama Sydney Stillbirth Study ambao ulisema ya kwamba wanawake wanaolala chali wakati wa ujauzito wako kwenye hatari ya mara sita zaidi ya kuzaa watoto wafu.
Utafiti huu wa Australia ulifanyika kwa miaka mitano na ulihusisha wanawake wajawazito 295 kutoka katika hospitali nane nchini Australia. Naye mtafiti mkuu katika utafiti huu Dr. Adrienne Gordon, kutoka Sydney's Royal Prince Alfred Hospital amesema “Tafiti za awali zilionyesha ya kwamba wanawake wanaolala chali wakati wa ujauzito, hupunguza mzunguko wa damu unaotakiwa kwenda kwa mtoto.Lakini pia ni vizuri kwa wanawake ambao ni wajawazito kutotaharuki kama wakati mwingine watalala chali.’’
Kutokana na idadi ndogo ya wanawake wajawazito waliohusishwa kwenye utafiti huu sisi wana Tanzmed tunachelea kusema ya kwamba ni vigumu kusema utafiti huu umetoa mapendekezo sahihi ya namna ya kulala kwa wanawake wajawazito.Pia kutokana na kutoangalia muda ambao wanawake hao walilala wakiwa chali (mfano kama walilala masaa 4,6 au 8 kwa siku na kwa siku ngapi) na tofauti ya hatari kati ya wanawake wajawazito waliolala muda mfupi na mrefu, hivyo tunawaambia wanawake wajawazito kutohofu kama watalala chali lakini ni bora kuchukua tahadhari mapema.Tafiti hii inatoa changamoto kwa watafiti wetu wa afya kuangalia jinsi ya kufanya tafiti kama hizi katika mazingira ya kwetu.