Watafiti hao wamedai kuwa, mamilioni ya watu ambao walikuwa wanatumia Aspirini katika kiwango hiki kwa ajili ya matibabu ya magonjwa ya moyo, wapo katika nafasi nzuri zaidi ya kuepuka kupata au kufa kutokana na magonjwa ya kansa.
Hata hivyo kumewahi kuwa na hofu huko nyuma kuhusu tabia ya Aspirini katika kusababisha vidonda vya tumbo au kutapika damu kunakoletwa na kukwanguliwa kwa ukuta wa tumbo kunako sababishwa na matumizi yaliyopitiliza ya dawa hii. Hata hivyo Prof. Peter Rothwell wa hospitali ya John Radcliffe jijini Oxford, ambaye aliongoza jopo la watafiti waliofanya utafiti huo anaamini kuwa faida za utumiaji wa Aspirini zinazidi madhara yake.
Prof Rothwell anasema “Matokeo haya ya utafiti wetu yanaonesha kuwa faida zitakazopatikana kwa kutumia Aspirini katika kupunguza vifo vitokanavyo na kansa zitapelekea kubadilishwa kwa kanuni zinazotawala matumizi yaliyozoeleka ya Aspirini.”
Matokeo ya utafiti huo yaliyochapishwa katika jarida la utafiti la The Lancet yalionesha kuwa kulikuwa na matokeo ya kuridhisha juu ya uwezo wa Aspirini katika kupunguza uwezekano wa kutokea kwa vifo vilivyosababishwa na kansa.
Ilionekana kuwa baada ya miaka mitano ya kutumia Aspirini, kiwango cha vifo kutokana na kansa kilipungua kwa asilimia 34 kwa aina zote za kansa zilizotafitiwa na asilimia 54 kwa kansa zinazoathiri mfumo wa chakula.
Hata hivyo ni idadi ya wanawake waliohusishwa katika utafiti huo ilikuwa ndogo kiasi cha kushindwa kutoa matokeo ya kuridhisha kuhusu uhusiano kati ya matumizi ya Aspirini na vifo visababishwavyo na kansa ya matiti kwa kina mama.