Image

Sababu na dalili za Kuharibika kwa Mimba - Sehemu ya Kwanza

Kuharibika kwa Mimba ni nini?

Utangulizi

Kuharibu/kuharibika kwa mimba kwa njia ya kutoa kiinitete (embryo) au mjusi (fetus) kabla ya kutimiza umri wa kuweza kuishi nje ya mfuko wa kizazi hujulikana kama abortion 1. Mimba inapoharibika yenyewe kabla ya kutimia umri wa wiki 20 hujulikana kama miscarriage.

Kuharibu mimba kwa kukusudia bila kuwepo kwa sababu za msingi za kitabibu zinazomruhusu mama mjamzito kufanya hivyo ndio hujulikana kama criminal abortion, ambayo kulingana na katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kosa la jinai (Criminal Act).
Katika makala hii nitaeleza kwa kina kuhusu kuharibika kwa mimba. Karibia mimba milioni 56 huharibika kila mwaka duniani kote 2 .

Kuharibika kwa mimba miezi mitatu ya mwanzo ya ujauzito (First Trimester Miscarriage)

Visababishi

a) Asilimia 50-70% ya mimba zote zinazoharibika zenyewe wakati wa miezi mitatu ya mwanzo ya ujauzito hutokana na matatizo ya kiasili au vina saba (genetics or chromosome abnormalities) kama;

  • Autosomal trisomy (22.3%)
  • Monosomy (8.6%)
  • Triploidy (7.7%)
  • Tetraploidy (2.6%)

b) Magonjwa yanayotokana na kinga ya mwili (Collagen Vascular Disease)-Magonjwa haya hutokana na mwili wa binadamu kutengeneza chembechembe za antigen ambazo hushambulia viungo vyake venyewe . Magonjwa haya ni Systemic Lupus Erythematosus (SLE) na Antiphospholipid Antibody Syndrome.

Magonjwa haya husababisha mimba kuharibika mara kwa mara chini ya umri wa miezi mitatu ya mwanzo.Hivyo ni muhimu mgonjwa anayepata tatizo la kuharibika mimba mara kwa mara kufanyiwa kipimo cha damu mapema ili kugundua uwepo wa magonjwa haya na kupewa tiba stahiki.


c) Kukosekana kwa uwiano wa vichocheo (Hormonal imbalance) kama cushing syndrome, ugonjwa wa tezi koo ( thyroid diseases,) Polycystic ovary syndrome na Luteal Phase Defect.
Luteal Phase Defect - Ni upungufu wa kichocheo aina ya progesterone ambacho ni muhimu sana katika ukuaji wa mimba.

Ugonjwa huu pia huweza kugundulika kwa kipimo cha damu au kipimo cha kuchukua chembechembe za kuta za kizazi na baadae kuzipeleka maabara kwa ajili ya kuzipima. Mgonjwa hutibiwa kwa kupewa vidonge (supplement) vya kuongeza kichocheo hiki pungufu aina ya progesterone.

d) Matatizo katika maumbile ya mfuko wa uzazi (Uterine malformations) kama;

  • Septate uterus
  • Unicornuate uterus
  • Bicornuate uterus
  • Intrauterine adhesions

e) Uvimbe katika mfuko wa kizazi (Fibroids)
f) Kulegea kwa shingo ya kizazi (Cervical incompetence)

g) Mama mwenye kinga ya mwili dhaifu (Immunity problems) inayoshindwa kulinda kiumbe kilichomo kwenye mfuko wa kizazi dhidi ya uvamizi unaoweza kuambatana na vimelea vya asili vya baba mtoto

h) Trauma - Madhara ya kimwili ambayo yanaweza kusababisha kuharibika kwa mimba mapema ni pamoja na kufanya kazi kwa muda mrefu kupitiliza, kufanya kazi ngumu, kupigwa kwa mjamzito kwenye tumbo. Kukosekana kwa utulivu wa kiakili pia ni mojawapo wa chanzo cha kuharibika kwa mimba kwa mfano, kupatwa na hofu, uoga,      huzuni, msongo wa mawazo nk.

i) Sababu za kimazingira kama madhara yatokanayo na sumu ya arsenic, madini ya risasi, dawa za kuua wadudu mashambani (pesticides), formaldehyde nk.

j) Uvutaji sigara na unywaji pombe - Wajawazito wanaovuta sigara au kunywa pombe wapo kwenye hatari mara mbili ya kuharibikiwa kwa mimba wakilinganishwa na wajawazito wasiokunywa pombe au kuvuta sigara

k) Matumizi ya dawa kiholela kipindi cha ujauzito pasipo maelekezo ya daktari - Dawa za maumivu za jamii ya Non-steroidal anti-inflamatory drugs (NSAIDS), dawa aina ya retinol ambazo hutumiwa kutibu magonjwa ya ngozi kama chunusi na eczema na dawa zinazotumiwa kutibu ugonjwa wa baridi yabisi (rheumatoid arthritis).

Dawa hizi jamii ya NSAIDS husababisha kuharibika kwa mimba kwa kuyumbisha viwango vya vichocheo (hormones) mwilini. Mamlaka ya chakula na dawa ya Marekani (FDA) katika ripoti yake ya mwaka 2011 imesema matumizi ya dawa aina ya ibuprofen kipindi cha umri wa miezi mitatu ya ujauzito yanahusishwa na kuzaa mtoto mwenye  matatizo ya moyo, kupungua kwa maji ya uzazi (oligohydromnios) na kusababisha mama mjamzito kupata uchungu wa kujifungua kwa muda mrefu sana (prolonged labour) .

l) Uzito uliopitiliza (obesity) - Ni mojawapo wa chanzo cha kuharibika kwa mimba katika kipindi hiki cha miezi mitatu ya mwanzo ya ujauzito.

m) Utapia mlo (Malnutrition) - Utapia mlo kwa mama mjamzito uhusishwa moja kwa moja na kuharibika kwa mimba kwa sababu ya ukosefu wa virutubisho muhimu kwa kiumbe kilichomo ndani ya mfuko wa kizazi.

n) Unywaji wa kinywaji chenye caffeine zaidi ya 200mg kwa siku huchangia kuharibika kwa mimba katika kipindi hiki cha ujauzito. Kikombe kimoja cha chai (mug of tea) kina ujazo wa 75mg ya caffeine.Vilevile kikombe kimoja cha chai (mug of tea) iwapo mnywaji anatumia instant coffee, kina ujazo wa 100mg ya caffeine. Caffeine pia hupatikana kwenye vinywaji baridi kama coca cola, pepsi, kwenye vinywaji vya kuongezeka nishati mwilini (energy drinks) na kwenye chokoleti.

o) Umri mkubwa-Wanawake wanaoshika mimba kwa mara ya kwanza wakiwa na umri mkubwa wapo kwenye hatari ya kupata tatizo hili la kuharibika kwa mimba.

  • Kwa wanawake walio na umri chini ya miaka 30- Mimba 1 kati ya 10 huharibika
  • Kwa wanawake walio na umri kati ya miaka 35 hadi 39- Mimba 2 kati ya 10 huharibika
  • Nusu ya mimba zote za wanawake mwenye umri wa miaka 45 na kuendelea huishia kuharibika.

Wanawake wanaoshika mimba mara ya kwanza wakiwa na umri mkubwa wa miaka 30 na kuendelea wapo kwenye hatari kubwa ya kupata mtoto mwenye matatizo ya kuzaliwa (congenital malformations) na hivyo kuwa na uwezekano mkubwa wa mimba hiyo kuharibika.

Dalili za kuharibika kwa mimba

  • Kutokwa damu kwenye tupu ya mwanamke ambapo huanza kama matone na baadae kuongezeka kuwa nyingi
  • Maumivu ya tumbo chini ya kitovu
  • Homa
  • Ulegevu (weakness)
  • Maumivu ya kiuno (back pain)

Sababu zinazochangia mimba kuharibika kati ya miezi mitatu hadi sita ya Ujauzito (Second trimester miscarriage)

Kuharibika kwa mimba katika kipindi cha wiki ya 12 hadi 20 hujulikana kama second trimester miscarriage. Ni asilimia 2-3 ya mimba huharibika katika kipindi hiki cha ujauzito. Sababu za kuharibika kwa mimba kwa kipindi hiki ni kama zifuatazo

  • Magonjwa ya muda mrefu kama kisukari, ugonjwa wa shinikizo la damu, Sytemic Lupus Erythromatosus, magonjwa ya figo, magonjwa ya tezi la koo (hypothyroidism au hyperthyroidism).
  • Maambukizi kama rubella (german measles), cytomegalovirus, Bacterial Vaginosis, ugonjwa wa ukimwi, Chlamydia, kisonono (gonorrhea), kaswende (syphilis) na ugonjwa wa malaria. Mbali na kuharibu mimba, kaswende husababisha mjamzito kujifungua kiumbe mfu (stillbirth) na pia mtoto huzaliwa na maambukizi hatari ya ugonjwa        huu wa kaswende (congenital syphilis)
  • Uvimbe kwenye mfuko wa kizazi (fibroids)
  • Uvimbe kwenye mayai ya mwanamke (Polycystic Ovarian Syndrome, PCOS)
  • Matatizo kwenye shingo ya kizazi (Cervical Insufficiency)
  • Historia ya upasuaji wa shingo ya kizazi (Previous cervical surgery)
  • Kuwepo kwa kifafa cha mimba (Early pre-eclampsia or eclampsia)
  • Matumizi ya madawa ya kulevya kama cocaine nk.
  • Matatizo ya maumbile ya mfuko wa kizazi (Abnormal shape of the uterus)
  • Trauma - Madhara ya kimwili ambayo yanaweza kusababisha kuharibika kwa mimba mapema ni pamoja na kufanya kazi kwa muda mrefu kupitiliza, kufanya kazi ngumu, kupigwa kwa mjamzito kwenye tumbo.
  • Kukosekana kwa utulivu wa kiakili pia ni mojawapo wa chanzo cha kuharibika kwa mimba kwa mfano, kupatwa na hofu, uoga,     huzuni, msongo wa mawazo nk.
  • Sumu kwenye chakula (Food poisoning) kama Listeriosis, Toxoplasmosis , Salmonella nk.

Dalili za kuharibika mimba katika kipindi hiki?

Dalili hizi ni kama zifuatazo

  • Kutokwa damu kwenye tupu ya mwanamke
  • Maumivu makali ya chini ya kitovu
  • Kutohisi mtoto akicheza ndani ya tumbo la mama mjamzito

Fikra potofu kuhusu mimba kuharibika (Misconceptions about miscarriage)

Kumekuwepo na fikra nyingi potofu ambazo zinahusishwa na kuharibika kwa mimba.

Zifuatazo ni baadhi ya fikra hizo potofu ambazo ni

  • Kufanya mazoezi wakati wa ujauzito
  • Kunyanyua vitu au kujikamua wakati wa ujauzito
  • Kusafiri kwa kutumia ndege
  • Mama mjamzito kufanya kazi huku amesimama au amekaa kwa muda mrefu
  • Kushtuka kipindi cha ujauzito (shock or fright)
  • Kula vyakula venye pilipili
  • Kujamiana (tendo la ndoa) isipokuwa pale mama mjamzito anapokuwa na dalili za mimba inayotishia kutoka (threatened abortion), ndio hashauriwi kufanya tendo la ndoa.

Fikra tajwa hapo juu hazihusiani kabisa na kuharibika kwa mimba.

Marejeo
1. Grimes, DA; Stuart, G (2010). "Abortion jabberwocky: the need for better terminology". Contraception. 81 (2): 936. doi:10.1016/j.contraception.2009.09.005. PMID 20103443
2. Sedgh, Gilda; Bearak, Jonathan; Singh, Susheela; Bankole, Akinrinola; Popinchalk, Anna; Ganatra, Bela; Rossier, Clémentine; Gerdts, Caitlin; Tunçalp, Özge; Johnson, Brooke Ronald; Johnston, Heidi Bart; Alkema, Leontine (May 2016). "Abortion incidence between 1990 and 2014: global, regional, and subregional levels and trends". The Lancet. 388: 258–67. doi:10.1016/S0140-6736(16)30380-4. PMID 27179755
3. U.S. Food and Drug Administration's (FDA) 2011 Medication Guide for NSAIDs .


 Usikose sehemu ya pili ya makala hii wiki ijayo…

Imesomwa mara 46575 Imehaririwa Jumatatu, 11 Juni 2018 12:43
Dr Khamis

Dr. Khamis H.Bakari (MD PhD) ni daktari bingwa,mhadhiri katika chuo cha afya cha Chuo  Kikuu cha Dodoma,mtaalamu wa Tiba na Uchunguzi kwa kutumia mionzi ya nyuklia (Nuclear medicine).

Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.

Makala shabihana