Image

Kushindwa Kujizuia Kujikojolea

Tatizo hili la kujikojolea bila sababu yoyote ya msingi ni tatizo linaloathiri watu wengi sana na ambalo huleta usumbufu  na aibu kubwa kama litampata mtu. Tatizo hili huwakumba sana wanawake kuliko wanaume  na inakisiwa kuwa asilimia 35 ya watu walio na umri zaidi ya miaka 60 wana tatizo hili, kati ya hawa wanawake ni mara mbili ya wanaume wanaopata tatizo hili.

Hakuna uhusiano wowote wa tatizo hili na vitendo vya kujaamiiana kinyume cha maumbile au ngono kwa njia ya haja kubwa (anal sex) au ushoga (homosexuality).
 
Miongoni mwa sababu zinazochangia kutokea kwa tatizo hili ni
  • Jinsia – Hutokea zaidi kwa wanawake kuliko wanaume (stress incontinence), kutokana na ujauzito, kujifungua, wanawake ambao wameacha kupata hedhi (menopausal women) na maumbile ya kawaida ya mwanamke (normal  female anatomy), hata hivyo, urinary incontinence huwa zaidi kwa wanaume wenye matatizo ya kwenye tezi dume (prostate) kama saratani ya tezi dume,  uvimbe katika tezi dume (BPH) nk.
  • Umri  – Kutokana na kuongeza umri, muscle za kwenye kibofu cha mkojo na kwenye mrija wa kupitisha mkojo yaani urethra, zinaanza kuwa legevu (weak) na hivyo kusababisha mtu kushindwa kuzuia mkojo au kujikojolea. Hii haimanishi ya kwamba kila mtu ambaye ana umri mkubwa hupata tatizo hili, la hasha, linaweza kuonekana kwa baadhi tu ya watu wenye umri mkubwa. Mara nyingi huonekana kwa watoto wadogo au wachanga kutokana na kutokukomaa kwa viungo vyao (kibofu cha mkojo na mrija wa kupitisha mkojo)
  • Uzito uliopitiliza – Kuwa na uzito uliopitiliza (obesity) ni moja ya chanzo kinachochangia kutokea kwa tatizo hili kwani uzito huu huongeza shinikizo katika kibofu cha mkojo na kufanya muscle zinazozunguka kibofu hiki kuwa legevu na matokeo yake ni mtu kujikojolea pindi anapopiga chafya au kukohoa
.
  • Uvutaji sigara – Kikohozi  sugu kinachotokana na uvutaji sigara (chronic cough) pia huchangia kutokea kwa tatizo hili au kuongeza tatizo hili la kujikojolea kama lipo tayari. Kukohoa mara kwa mara, huongeza shinikizo kwenye milango (sphincters) ya mirija ya kupitisha mkojo na hivyo kusababisha tatizo la kujikojolea (stress incontinence). Na hii ndiyo sababu ambayo pia  inafanya kuonekana tatizo la kujikojolea kwa wagonjwa wa kifua kikuu, saratani ya mapafu na nk. Uvutaji sigara pia huchochea kwa kibofu cha mkojo  kusisimka kupita kiasi (overactive bladder) kutokana na  contractions zinazotokea kwenye kibofu cha mkojo.
  • Magonjwa mbalimbali kama magonjwa ya figo, kisukari, uvimbe katika tezi dume (BPH), saratani ya tezi dume (prostate cancer) na nk.
  • Nini chanzo cha tatizo hili?
    • Kukojoa mara kwa mara (polyuria) - Kutokana na magonjwa kama kisukari, kunywa vinywaji kwa wingi (primary polydipsia), diabetes insipidus (central na nephrogenic). Hali ya  kukojoa mara kwa mara huongeza hisia ya kutaka kukojoa (urgency)  na  vipindi vya  kukojoa kila wakati  (frequency) lakini haileti tatizo la kushindwa kuzuia kujikojolea.
    • Vinywaji vyenye caffeine na cola - Huchochea kibofu kutoa mkojo. (Kibofu ni kiungo cha kuhifadhi mkojo kwa muda tu ndani ya mwili kabla haujatolewa nje).Vinywaji kama soda, chai,kahawa, vinywaji vya kuongeza nishati mwilini (kama redbull nk), hata vinywaji vyenye viungo vingi (spicy) , sukari, na tindikali (acid) nyingi kama citrus na vya nyanya au tungule (tomatoes) pia huchochea kibofu cha mkojo kutoa mkojo.
    • Unywaji pombe – Pombe pia huchochea kibofu cha mkojo kutoa mkojo. Unywaji pombe kupitiliza humfanya mnywaji kushindwa kuzuia kutojikojolea lakini hii inakuwa kwa muda tu, pombe ikiisha mwilini mtu anarudi katika hali yake ya kawaida. Kwa wale ambao wamekuwa addicted na pombe, baada ya kunywa kwa kipindi kirefu ndio huweza kupata tatizo hili.
    • Uvimbe katika tezi dume kwa wanaume wenye umri zaidi ya miaka 40, husababisha tatizo hili la kujikojolea kama BPH, saratani ya tezi dume,  nk.
    • Dawa – Baadhi  ya dawa kama dawa za magonjwa ya moyo, dawa za shinikizo la damu (hypertensive medication), muscle relaxants, sedatives nk husababisha tatizo hili.
    • Tiba ya mionzi – Tiba za mionzi za saratani mbalimbali pia husababisha kutokea kwa tatizo la kushindwa kuzuia kujikojolea.
    • Magonjwa mbalimbali kama multiple sclerosis, kiharusi,maambukizi katika mfumo wa mkojo (UTI), kupata choo kigumu (constipation), spina bifida, parkinson’s disease na hata maumivu katika uti wa mgongo (spinal cord injury), saratani ya kibofu cha mkojo, ni moja ya chanzo cha tatizo hili.
    • Ujauzito -  Baadhi ya wanawake wajawazito na ambao wamejifungua hupatwa na tatizo la stress incontinence kutokana na mabadiliko ya viwango vya vichocheo mwilini (hormonal imbalance) pamoja na kuongezeka uzito kwa mfuko wa kizazi (enlargement of uterus). Msongo wa mawazo wakati wa kujifungua kwa njia ya kawaida huleta ulegevu wa muscle zinazohusika kusaidia kibofu cha mkojo katika kazi yake ya kuhifadhi na kutoa mkojo.
    • Tiba za upasuaji - Kama tiba ya kuondoa mfuko wa kizazi (hysterectomy)kutokana na magonjwa mbalimbali pia husababisha tatizo hili kutokana na kibofu cha mkojo na mfuko wa kizazi kuwa karibu ndani ya mwili wa mwanamke, hivyo, muscle na ligament ambazo zinazosaidia mfuko wa kizazi kuuweka katika sehemu yake ndizo pia  husaidia kuweka kibofu cha mkojo katika sehemu yake sahihi mwilini.
    Aina za  tatizo la kushindwa kujizuia kujikojolea (Urinary incontinence)
    Kuna aina nyingi za tatizo hili  kama zifuatavyo
    • Stress incontinence – Aina hii ya kujikojolea, hutokea baada ya mtu kukohoa, kucheka, kupiga chafya, kufanya mazoezi au kunyanyua vitu vizito.  Stress incontinence hutokea baada ya milango ya kibofu cha mkojo kuwa legevu (sphincter muscles). Huonekana wakati wa ujauzito, wakati wa kujifungua, na wakati mwanamke amesita kupata hedhi kutokana na umri kuwa mkubwa (menopause). Kwa wanaume, inaweza kutokea baada ya kuondoa tezi dume (prostate).
    • Urge incontinence – Hali inayotokea  ghafla ya kuhisi unahitaji kukojoa. Hali hii husababishwa na maambukizi katika mfumo wa mkojo (UTI), kiharusi, ugonjwa wa uzeeni wa kupoteza kumbukumbu (alzheimer’s disease), parkinson’s disease, multiple sclerosis, bowel irritants na nk.
    • Overflow incontinence – Hali ya kushindwa kuzuia mkojo kutoka mara kwa mara, mtu kila akijisaidia haja ndogo bado anahisi ya kwamba hajamaliza haja yake hiyo, kwa hiyo kila mara mtu hupata haja ndogo au mkojo unatoka.Hii hutokana na madhara kwenye kibofu cha mkojo (damaged bladder), madhara ya neva kutokana na ugonjwa wa kisukari, multiple sclerosis, maumivu katika uti wa mgongo.Kwa wanaume aina hii, huusishwa na matatizo katika tezi dume kama BPH, saratani ya tezi dume.
    • Mixed incontinence – Katika aina hii, mtu anakuwa na  aina  zaidi ya moja za urinary incontinence.
    • Functional incontinence -  Hii hutokea pale ambapo mtu anashindwa kwenda chooni kujisaidia haja ndogo kutokana na umri kuwa mkubwa au matatizo mengine ya afya kama kiharusi, ugonjwa wa mifupa aina ya arthritis na nk.
    • incontinence – Mtu anaweza kuwa na hali ya mkojo kumtoka  bila kuweza kuuzuia kwa wingi muda  wote  yaani mchana na  usiku  bila sababu yoyote.
    • Transient incontinence – Aina hii ya mkojo kutoka bila kuweza kuuzuia hutokea kwa muda tu (temporary) na husababishwa na baadhi ya dawa, adrenal insufficiency, mental impairement, au hali ya kushindwa kupata choo kutokana na choo kuwa kigumu sana (stool impaction due to severe constipation).
    • Giggle incontinence – Huwapata sana watoto wadogo wakati wanacheka na mkojo huwatoka ghafla. Mara nyingi mkojo unaotoka hapa unakuwa kidogo sana, na ni hali ya muda tu sio endelevu (temporary). Baadhi ya watoto hujikojolea wakati wapo usingizini na hujulikana kama bedwetting.
    • Coital Incontinence – Ni aina ya kupata haja ndogo wakati wa kujamiana au wakati wa kufikia kilele (orgasm) na inaweza kutokea wakati wa kujamiana kwa mwanamke na mpenzi wake au wakati wa kujichua (masturbation). Huonekana kwa wanawake.
    Vipimo vya Uchunguzi
    Ugunduzi wa tatizo hili utahusisha daktari kuchukua historia ya mgonjwa ambayo italenga kutambua aina ya dawa anazotumia au ambazo alishawahi kutumia, tiba ya upasuaji yoyote ambayo alifanyiwa hapo awali, ugonjwa wowote alionao mgonjwa, na kama ana historia ya kupata maumivu wakati wa kukojoa au kama anajikamua wakati anakojoa. Pia daktari atamfanyia uchunguzi mgonjwa ili aangalie kama kuna dalili na viashiria vyovyote vya ugonjwa wowote.
    Vipimo vya uchunguzi vitahusisha;
    • Vipimo vya damu (Complete Blood Count or FBP) – Kuangalia wingi wa damu na chembechembe mbalimbali za damu.
    • Urinalysis – Vipimo vya mkojo kuangalia kama kuna mawe katika figo, maambukizi katika njia ya mkojo (UTI) na nk.
    • Ultrasound ya kuangalia figo, kibofu cha mkojo, ureters na urethra.
    • Stress test –  Hapa daktari anamuhimiza mgonjwa kukohoa wakati huohuo akitazama  kama  kuna mkojo unaotoka wakati mgonjwa anakohoa.
    • Kipimo cha Cystoscopy – Mpira ulio na kamera ndogo kwa mbele huingizwa katika mirija ya kutoa mkojo (urethra) wa mgonjwa ili kutazama kama kuna matatizo yoyote ndani ya  urethra na kwenye kibofu cha mkojo.
    • Urodynamics – Vipimo mbalimbali vya kupima shinikizo ndani ya kibofu cha mkojo na shinikizo ya mkojo wenyewe.
    • Postvoid residual measurement (PVR) – Mgonjwa anakojoa katika chombo cha kupima wingi wa mkojo, na baada ya hapo daktari hupima kiwango cha mkojo uliobakia ndani kwa  kuingiza mpira au catheter katika mrija wa kupitishia mkojo na kuupima baada ya kutoka au anaweza kutumia kipimo cha ultrasound kuangalia kiwango cha mkojo kilichobakia.
    • Cystogram – Baada ya kuingiziwa mpira au catheter katika mrija wa kupitisha mkojo mpaka kwenye kibofu cha mkojo, rangi maalum (contrast dye) huingizwa katika mpira huu na mgonjwa hupigwa picha  za muda tofauti tofauti za x-ray ili kuangalia kama kuna tatizo lolote katika mfumo wa mkojo. 
    Tiba ya Urinary Incontinence
     
    Tiba ya kushindwa kujizuia kujikijolea ni kama ifuatavyo
    • Kubadilisha tabia ya kujisaidia haja ndogo (kukojoa) kwa
      1. Kufanya mazoezi ya kibofu cha mkojo - Wakati mtu anahisi haja ya kukojoa basi anashauriwa ajizuie kwa angalau dakika 10 halafu ndio aende kukojoa, lengo ni kurefusha zaidi muda huu wa kusubiri kukojoa hapo mbeleni. Au kama mtu akiwa na hisia ya kutaka kukojoa basi anaweza kukojoa kidogo tu halafu asubiri kidogo kabla ya kuendelea tena kukojoa.
      2. Kupanga muda maalum wa kwenda chooni kukojoa na usisubiri mpaka huhisi kutaka kukojoa
      3. Kubadilisha aina ya vinjwaji mgonjwa anavyotumia, kuacha kutumia vinywaji venye caffeine, cola, vinywaji venye viungo vingi (spicy), sukari na tindikali nyingi (acid) kama citrus, carbonated drinks na nk.
      4. Kufanya mazoezi ya pelvic muscles (kegel exercise) kwa kufanya kama unazuia mkojo wakati unahisi haja ndogo na kuhesabu kutoka moja hadi tano, baada ya tano pumzika na halafu rudia. Mazoezi haya huongeza ukakamavu katika sehemu za nyonga pamoja na muscles za nyonga na hivyo kusaidia kuweza kuzuia mkojo.
      5. Electrical stimulation – Kwa kutumia electrodes ambazo huingizwa kwenye njia ya haja kubwa kupitia kwenye puru (rectum) au kwenye tupu ya mwanamke (vagina) ili kuchochea  na kuleta ukakamavu wa muscles za pelvic au nyonga. Tiba hii huchukua muda mrefu na si tiba ya siku moja na hutumiwa kwa wale wenye  msongo wa mawazo na urge incontinence.
    • Vifaa maalum vya kusaidia kufyonza mkojo kama absorbent pad, condom catheter (mipira wanaovaa wanaume kama kondomu), chupi maalum (protective underwear), diapers, male urinary incontinence clamp, na nk. Hizi husaidia kufyonza mkojo au kuzuia mtu kujichafua kutokana na kujikojolea (haja ndogo) na hivyo kumuepusha na aibu au usumbufu anaopata mgonjwa.
    • Pessary – Ringi maalum ambayo mwanamke huivaa ndani ya tupu yake na hivyo kukisukuma kibofu cha mkojo ambacho kipo karibu na tupu yake juu zaidi na hivyo kuzuia mtu kujikojolea. Ringi hii huvaliwa kwa muda wa siku nzima, na mgonjwa atahitaji mara kwa mara kuitoa na kuisafisha au kama si hivyo basi atakuwa kwenye hatari ya kupata madhara kama maambukizi katika njia ya mkojo, PID (Pelvic Inflammatory Disease) na nk. Ringi hii huwasaidia sana wanawake walio na matatizo ya kuanguka kwa kibofu cha mkojo (prolapse urinary bladder)  au mfuko wa uzazi (prolapse uterus).
    • Tiba ya dawa – Dawa aina za anticholenergic kama oxybutynin (Ditropan), tolterodine (Detrol) na nk, husaidia wale wenye urge incontinence. Dawa za kupaka aina ya  topical oestrogen (cream) husaidia kupunguza dalili za tatizo hili. Imipramine hutumiwa kutibu mixed incontinence. Dawa aina ya Duloxetine inayotumiwa kutibu sonono (antidepressant) pia huweza kutumika kutibu stress incontinence. Ni vizuri kupata ushauri wa daktari pamoja na yeye kukupima kabla ya kuanza kutumia dawa hizi. Mara nyingi ni vigumu kutambua ni aina ipi ya  kushindwa kujizuia kujikojolea (urinary incontinence) mgonjwa aliyonayo isipokuwa daktari tu. Tiba za kuchoma sindano kama bulking material injections, Botulin toxin type A injections na nerve stimulators pia hutumika.
    • Tiba ya Upasuaji -  Kuna aina mbalimbali za tiba ya upasuaji kama;
      1. Sling procedures – Hii hutumia tishu za sehemu nyingine ya mwili wa mgonjwa, synthetic material or mesh ambazo hufungwa kwenye shingo ya kibofu cha mkojo na urethra, na husaidia kufunga urethra wakati mgonjwa anakohoa ama kupiga chafya.
      2. Bladder neck suspensions – Hufanywa kutoa msaada kwa urethra na shingo ya kibofu cha mkojo.
      3. Artificial urinary sphincter - Sphincter ya kutengeneza ambayo huvikwa kwenye shingo ya kibofu cha mkojo kwa wanaume walio na sphincter legevu kutokana na tiba ya saratani ya tezi dume au tiba ya uvimbe wa tezi dume (BPH).
    Bonyeza link zifuatazo ili kuweza kupata ufahamu zaidi kuhusu saratani ya tezi dume, saratani ya kibofu cha mkojo, na Uvimbe wa Tezi Dume (BPH) na kuona uhusiano wake na tatizo hili.
     
    Imesomwa mara 16001 Imehaririwa Jumatatu, 18 Novemba 2019 17:24
    Dr Khamis

    Dr. Khamis H.Bakari (MD PhD) ni daktari bingwa,mhadhiri katika chuo cha afya cha Chuo  Kikuu cha Dodoma,mtaalamu wa Tiba na Uchunguzi kwa kutumia mionzi ya nyuklia (Nuclear medicine).

    Anwani ya barua pepe hii inalindwa kutokana na spambots. JavaScript lazima iwe itawezeshwa kwa kuweza kuona.