Print this page
Mapishi ya Futari 3
Mapishi

Mapishi ya Futari 3

Mapishi ya futari za Ramadhani hayakamiliki bila kupika vibibi, shurba ya nyama ya mbuzi, mkate wa mofa, bokoboko la kuku na mihogo.

Mkate wa Mofa (Yemen)

 

 

 

 

 

 

 

Vipimo

Unga wa mahindi 1 mug

Unga wa mtama 2 mugs

Kitunguu maji 1 Kikubwa

Chumvi 1 Kijiko cha chai (Kidogo)

Sukari 1 Kijiko cha chakula

Hamira 1 Kijiko cha chai

Maji 3 mugs

Namna ya Kutayarisha na Kupika

  • Upike unga wa mahindi kama uji kwa dakika kama tano na maji mug mbili.
  • Uache upoe tia unga wa mtama na vitu vyote vilivyobaki pamoja na ile mug moja ya maji iliyobaki.
  • Uache mpaka uumuke.
  • Fanya maduara duara halafu tandaza uchome kwa moto mdogo kama chapati bila ya mafuta kwenye kikaango (frying pan). Choma mmoja mmoja yote hadi umalize..
  • Lipange kwenye sahani tayari kwa kuliwa na mchuzi wa nazi wa samaki au kuku au vyovyote upendavyo.

Muhogo, Samaki wa Kuchoma na Bamia

 

 

 

 

 

 

 

 

Vipimo

Mihogo (fresh) 3 - 4

Tui la kopo au (box) 1000 ml

Chumvi 1 kijiko cha chai

Kitunguu maji kilokatwakatwa 1

Nyanya mshumaa/tungule) 3-4

Pilipili mbichi ndefu 2-3

Pilipili boga 2

Namna ya Kutayrisha na Kupika

  • Menya mihogo kisha ikate kate vipande inchi tatu hadi nne, kila kipande kigawe kitoke vipanda vinne. Toa mzizi katikati.
  • Osha mihogo ipange kwenye sufuria ya nafasi na yenye mfuniko, ili upate nafasi ya kutia viungo unavyoona pichani na utokotaji wa tui wahitaji nafasi.
  • Panga/tandaza kitunguu, nyanya mshumaa/tungule, pilipili mbichi na pilipili boga juu ya mihogo, tia chumvi na tui lote.
  • Funika sufuria kisha weka jikoni moto wa kiasi kuchemsha tui lipande juu. Hakikisha tui halifuriki na kumwagika kwa kuchungulia au kufunika nusu mfuniko
  • Kwa muda wa nusu saa hivi ukiona sasa tui linatokota chini chini funika mfuniko na upunguze moto mdogo kabisa tui likauke kidogo na liwe zito.
  • Toa muhogo mmoja ubonyeze ukiona umeiva zima jiko na wacha sufuria hapo kwa muda wa dakika 10. Mihogo iko tayari kuliwa.

Kidokezo

Tui lote huwa chini baada ya mihogo kuiva unapopakuwa teka kutoka chini uweze kupata uzito wa tui umwagie juu.

Bamia/Mabenda

Vipimo

Bamia Robo kilo

Nyanya/Tungule 3

Kitunguu maji 1

Thomu ya unga au ilosagwa 1 Kijiko cha chai

Nyanya kopo (tomato paste) 1 Kijiko cha supu

Mafuta 150 ml

Chumvi 1 Kijiko cha chai

Pilipili boga 1

Namna ya Kutayarisha na Kupika

  • Kata vichwa vya bamia kisha zikate kate mara mbili zikiwa kubwa, ikiwa ni ndogo mno haina lazima kuzikata osha tu uweke kando.
  • Katika sufuria, katakata kitunguu, nyanya, pilipili boga tia ndani viungo hivi ongeza chumvi, mafuta, thomu na nyanya kopo
  • Washa moto mdogo mdogo huku umefunika sufuria kwa muda wa dakika 20 kisha ukiona mboga zimeshika kutokota ongeza bamia koroga.
  • Tia maji 200ml (glasi 2) wacha kwa muda wa dakika 15 kupikika tena, ukionja utamu wa mboga na chumvi, hakikisha bamia pia zimeiva. Hapa Bamia zipo tayari kuliwa.

Samaki wa Kuchoma

Vipimo

Samaki (dorado) au mikizi au tuna 2 Wakubwa (fresh)

Chumvi 1 Kijiko cha chai

Thomu ya unga au iliyosagwa 1 ½ cha chai

Tangawizi mbichi iliyosagwa 1 Kijiko cha supu

Namna ya Kutayrisha na Kuchoma

  • Safisha samaki vizuri mchane chane (slit) kwa ajili ya kuweka masala.
  • Changanya viungo vyote na chumvi, kisha paka katika samaki nje na ndani na sehemu ulizochanachana. Mloweke kwa muda wa robo saa hivi.
  • Weka karatasi ya jalbosi (foil paper) katika tray (treya) ya oveni. Muweke samaki kisha mpike (grill) kwa moto wa juu achomeke hadi samaki agueke rangi na aive.

Kidokezo

Kuweka karatasi ya jalbosi katika tray ya oveni kunasaidia kuhifadhi tray kuchafuka na tabu ya kusugua na kuiosha.

Hariys - Bokoboko la Kuku

 

 

 

 

 

 

 

Vipimo

Ngano nzima (shayiri) 3 Vikombe

Kuku ½ (3 lb au kilo moja na nusu)

Thomu na tangawizi iliyosagwa 1 Kijko cha supu

Pilipili manga ya unga ½ Kijiko cha chai

Jiyrah (cumin/bizari ya pilau) ½ Kijiko cha chai

Chumvi Kiasi

Kidonge cha supu (Curry cube) 1

Samli ya moto ½ Kikombe

Namna ya Kutayarisha na Kupika

  • Loweka ngano (shayiri) tokea usiku au muda wa masaa.
  • Katakata kuku mtie katika sufuria, tia maji kiasi na viungo vyote. Mchemeshe aive na ibakie supu yake.
  • Toa kuku, toa mifupa na umchambue chambue vipande vidogo vidogo.
  • Chemsha ngano (shayiri) kwa kufunika sufuria hadi iive na kukauka maji.
  • Tia supu ya kuku katika ngano (shayiri), na kuku uliyemchambua. Tia kidonge cha supu (curry cube)
  • Tia samli nusu (bakisha nusu) kisha changanya mchanganyiko hadi uvurugike kuku na ngano (shayiri) vizuri.
  • Mimina katika sahani, mwagia samli ya moto iliyobakia ikiwa tayari.

Kidokezo

Ukipenda kulia na sukari

Shurba ya Nyama ya Mbuzi

 

 

 

 

 

 

 

Vipimo

Nyama ya mbuzi 2lb (Kilo moja)

Nyanya 1

Kitunguu maji 1

Kidonge cha supu (curry cube) 1

Maji 4 Mugs

Thomu 1 Kijiko cha supu

Bizari ya pilau (cumin) 1 Kijiko cha chai

Bizari ya manjano ½ Kijiko cha chai

Mdalasini 1 Kijiti

Shairi (oats) 5 Vijiko supu

Pilipili mbichi 2

Siki ya zabibu (Grape vinegar) 2 Vijiko vya supu

Chumvi Kiasi

Namna ya Kutayarisha na Kupika

  • Osha nyama vizuri tia kwenye sufuria.
  • Katakata kitunguu na nyanya, ikiwa hupendi maganda ya nyanya toa na ukate kate.
  • Tia kidonge cha supu, mdalasini, chumvi na maji funika uchemshe nyama mpaka iive.
  • Tia shairi (oats) kwenye bakuli na maji iache, nusu saa kisha isage kidogo tu, na mimina kwenye supu ya nyama.
  • Tia pilipili mbichi nzima, thomu, bizari zote na siki. Weka moto mdogo mdogo huku unakoroga kila baada ya muda.
  • Tazama uzito, na ongeza maji kidogo ikiwa nzito sana

Kidokezo

Ikiwa huna siki ya zabibu tia ndimu au limao au white vinegar.

Vibibi

 

 

 

 

 

 

 

Vipimo

Mchele 2 Vikombe

Tui la nazi 1 1/2 Kikombe

Mafuta 1 Kijiko cha supu

Hamira 2 Vijiko vya chai

Unga wa ngano 1 Kijiko cha supu

Hiliki Kiasi upendavyo

Sukari ¾ au 1 Kikombe

Namna ya Kupika na Kutayarisha

  • Osha na loweka mchele usiku mzima ndani ya maji baridi.
  • Mimina vifaa vyote isipokuwa sukari , ndani ya mashine ya kusagia (blender) na usage mpaka mchele uwe laini.
  • Mimina ndani ya bakuli na ufunike , kisha weka pahali penye joto ili mchanganyiko ufure/uvimbe.
  • Ukishafura , mimina sukari na changanya vizuri ; ukiona mchanganyiko ni mzito sana, ongeza maziwa kidogo.
  • Weka chuma kipate moto.
  • Paka mafuta au samli kidogo kwenye chuma kisha mimina mchanganyiko kiasi kuunda duara na ufunike.
  • Utazame ikishaiva upande mmoja , geuza upande wa pili mpaka iwe tayari.
  • Endelea Mpaka umalize mchanganyiko wote; panga kwenye sahani na tayari kuliwa.

Kidokezo

Unaweza kutumia chuma kisichoganda ( non stick ); nacho hakitaraji kutiwa mafuta.

Vibibi vya Tui la Nazi

 

 

 

 

 

 

Vipimo

Mchele 2 Vikombe

Tui la nazi zito 2 Vikombe

Hamira 1 Kijiko Cha chai

Unga wa ngano 2 Vijiko vya supu

Iliki Kiasi upendavyo

Sukari Kiasi upendavyo

Yai 1

Vipimo vya Tui la Kupaka

Tui la nazi 2 Vikombe

Hiliki ya unga Kiasi upendacho

Sukari Kiasi upendacho

Unga wa ngano 1 Kijiko cha supu

Namna ya Kutayarisha na Kupika

  • Changanya vitu vyote vya tui la kupaka katika kisufuria kidogo.
  • Lipike tui huku walikoroga mpaka lichemke na liwe zito.
  • Osha na loweka mchele usiku mzima ndani ya maji baridi.
  • Mimina vifaa vyote isipokuwa yai na sukari , ndani ya mashine ya kusagia (blender) na usage mpaka mchele uwe laini.
  • Mimina sukari na yai usage kidogo tu kiasi cha kuchanganya.
  • Mimina ndani ya bakuli na ufinike , kisha weka pahali penye joto ili mchanganyiko ufure/uvimbe
  • Ukishafura, weka chuma kipate moto. (Ni bora kutumia kichuma kidogo)
  • Katika sahani ya kupakulia, paka tui kote.
  • Tia kijiko nusu cha chai cha mafuta au samli kwenye chuma kisha mimina mchanganyiko ukitumia upawa na ufunike.
  • Kibibi kikianza kuiva na kushikana upande mmoja , kigeuze upande wa pili mpaka kigeuke rangi na kuiva.
  • Panga kwenye sahani iliyopakwa tui.
  • Endelea Mpaka umalize mchanganyiko wote; kila ukiepua kibibi, panga juu ya mwenzake kama ilivyo kwenye picha na upake tui juu yake.

Usikose makala zifuatazo za mahanjumati ya Eid.

Shukrani kwa tovuti ya www.alhidaaya.com kwa makala hii.

Imehaririwa Jumanne, 09 Juni 2020 11:49
Tagged under
Share
Dr Khamis

Dr. Khamis H.Bakari (MD PhD) ni daktari bingwa,mhadhiri katika chuo cha afya cha Chuo  Kikuu cha Dodoma,mtaalamu wa Tiba na Uchunguzi kwa kutumia mionzi ya nyuklia (Nuclear medicine).

Makala zaidi kutoka kwa Dr Khamis

Makala shabihana